Rais wa Tanzania John Magufuli amewasihi
Watanzania kuwapuuza watu aliosema wanataka
kutumia maafa yaliyotokana na tetemeko la
ardhi eneo la Kagera kuchochea chuki dhidi ya
serikali.
Mikoa jirani ya Mwanza, Geita na Mara pia
iliathirika.
Dkt Magufuli amesema hata mataifa makubwa
yenye maendeleo makubwa ya uchumi na
teknolojia yanakumbwa na mitetemeko ya ardhi
na kusababisha vifo vya idadi kubwa ya wananchi
na uharibifu mkubwa wa mali.
Akiongea mwishoni mwa wiki, rais huyo alisema
mpaka sasa hakuna teknolojia ya kutabiri kutokea
kwa tetemeko la ardhi na kwamba tetemeko hili
halikuletwa na Serikali.
Tetemeko: Waathiriwa waomba msaada
Tanzania
Kwa Picha: Tetemeko la ardhi Tanzania
"Nilikuwa najaribu kuangalia kwa mfano nchi
kama China kwenye mwaka 2014 watu 617
walipoteza maisha, mwaka 2013 walipoteza watu
193, Mwaka 2010 walipoteza watu 2,998 mwaka
2008 China ilipoteza watu 98,712," alisema kwa
mujibu wa taarifa kutoka ikulu.
"Ukijaribu kuangalia Japan, nchi ambayo
imeendelea na ina utaalamu wa hali ya juu sana,
kwenye mwaka 2016 tarehe 14 mwezi wa nne
ilipoteza watu 6, baada ya siku mbili tarehe 16
mwezi wa nne 2016 tetemeko likatokea tena na
likaua watu 35 … mwaka 1923 liliua watu
142,800 na hiyo ni Japan."
Rais Magufuli alisema hayo Jumamosi katika
ikulu ya Dar es Salaam alipokuwa akipokea
mchango wa fedha taslimu kiasi cha Dola za
Kimarekani laki mbili (Tshs 437 milioni) kutoka
kwa Rais wa Uganda Yoweri Kaguta Museveni
kusaidia walioathiriwa na tetemeko hilo lililotokea
wiki moja iliyopita.
Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta alituma mchango
wa mabati, blanketi na magodoro vyenye thamani
ya shilingi za Kitanzania milioni 115 kuwasaidia
waathiriwa.
Watu 17 walifariki, 440 wakajeruhiwa na nyumba
2,063 zikabomoka kutokana na tetemeko hilo kwa
mujibu wa serikali ya Tanzania.
Nyumba 14,081 zipo katika hali hatarishi na
nyumba 9,471 zimepata uharibifu mdogo, huku
watu 126,315 wakihitaji misaada mbalimbali.
Rais Magufuli ameahidi kuwa Serikali itahakikisha
inarekebisha miundombinu iliyoharibika lakini
akawataka wananchi wajipange kurekebisha
nyumba zao kwa kuwa Serikali pekee yake
haitaweza kujenga nyumba zote zilizobomoka.
Kwa mujibu wa Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim
Majaliwa, kufikia mwishoni mwa wiki shilingi za
Kitanzania bilioni tatu nukta sita (dola 1.6
milioni) zilikuwa zimepatikana za kuwasaidia
waathiriwa.
No comments:
Post a Comment